MBUNGE wa Lindi Mjini, Salum Barwani, ametakiwa kuachana na
Chama cha Wananchi (CUF) na badala yake ajiunge na Chama cha Demokrasia
na Maendeleo (CHADEMA) ili aweze kuwatumikia wananchi ipasavyo.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Mwenyekiti wa Taifa wa CHADEMA, Freeman
Mbowe wakati akijibu kero mbalimbali za wananchi wa Kata ya Ng’apa
katika Jimbo la Lindi Mjini na kusema ndani ya CUF, Barwan ataendelea
kuwa mtumwa wa maamuzi ya viongozi wake pasipo kuwatumikia wananchi.
Maamuzi ya Mbowe kumkaribisha Barwan, yalitokana na malalamiko ya
wananchi kuwa jitihada za mbunge huyo kuwatumikia zinakwamishwa na
viongozi wa serikali pamoja na madiwani wa mkoa huo, na kwamba viongozi
wa CUF Taifa wanashindwa kumsaidia katika vita hiyo.
Mbowe alisema katika mazingira ya CUF, Barwan ataendelea kutaabika kwa
kuwa viongozi wake wa kitaifa wameamua kumsusa kwa kufunga ndoa na
Serikali ya CCM, hivyo hatoweza kusimamia maslahi ya wananchi.
“Sina ugomvi na Barwan, tunafanya nae kazi vizuri ila misimamo ya
viongozi wake wakuu ni tatizo kwake, ninamshauri ajitathmini, na huku
kwetu mlango uko wazi, anaweza kuusukuma na kuingia kwa ajili ya
kuwatetea wana Lindi,” alisema Mbowe.
Kauli hiyo ilionekana kumchoma aliyekuwa mpiga debe wa mbunge huyo,
Abdallah Madebe, ambaye alikiri kuwa hatima ya CUF haieleweki na hataki
chama hicho kimfie mikononi.
Kutokana na hilo, Madebe aliamua kujiondoa katika chama hicho na
kutangaza kujiunga na CHADEMA, hivyo kupokelewa rasmi na Mbowe.
Malalamiko mengine ya wananchi hao yalikuwa katika suala zima la
mfumuko wa bei, kukosa huduma za afya na wanafunzi kutozwa shilingi
20,000, kwa ajili ya ulinzi wa shule za serikali.
Mkazi wa Ng’apa, Rashid Issa ‘Mbele wapi’, alisema hawajui hatma ya
nchi yao kwa kuwa na maisha yao kutokana na mfumuko wa bei unaojitokeza
kila wakati, huku wakiendelea kutozwa kodi katika vivuko vya mazao na
fedha hizo kuishia mikononi mwa wajanja.
Akijibu hoja hizo, Mbowe alisema maisha magumu kwa Watanzania ni
matokeo ya sera mbovu za Serikali ya CCM juu ya kusimmia uchumi wa nchi.
Kuhusu matatizo ya wananchi, Mbowe aliwataka wakazi wa Lindi
kutowavumilia viongozi wazembe ambao hawawezi kuwaelezea kodi zao
zilivyotumika wakati wao wanashindwa kupata huduma za msingi.
Dk. Slaa awavaa askari uwanjani
Akizungumza katika mkutano uliofanyika katika Uwanja wa Ilulu mkoani
hapa, Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willbroad Slaa aliwataka askari polisi
wasipate tabu ya kurekodi mikutano yao bali fedha wanazonunulia kanda
za kurekodia wazitumie kuboreshea maisha yao.
Alisema katika mikutano ya CHADEMA, askari wanajaa kwa wingi kwa lengo
la kusikiliza vitu gani vinaongelewa ili wawafikishie mabosi wao, ambao
hawawajali kimaslahi na kuwaacha wakiendelea kutaabika kwa hali ngumu,
huku wengine wakiendelea kukaa katika nyumba za bati maarufu kama ‘full
suti’.
“Ninyi maaskari mnanishangaza sana, ufisadi umejaa kila sehemu, badala
ya kushughulika na hayo, ninyi mnakuja kurekodi ili mseme tunachochea
vurugu, sasa ninawaambia nina barua ya viongozi wenu kwenda kwa rais,
ikimlalamikia RPC aliyeondoka wa mkoa huu kwa kufanya ufisadi wa milioni
34 kisha akaondoka kabla ya kuchukuliwa hatua,” alisema Dk. Slaa.
Alisema atakachoweza kuwasaidia askari ni kuhakikisha kuwa mishahara
yao inaongezwa baada ya mwezi wa saba, vinginevyo Rais Kikwete ajiandae
kwa kuipokea nguvu ya umma kwa ajili ya kudai maslahi ya walimu na
askari pamoja n watumishi wengine.
Dk. Slaa alisema kama kuna watu wanaostahili kukamatwa au kufuatiliwa,
ni Mkuu wa Polisi nchini pamoja na Waziri Khamis Kagasheki ambaye kwa
sasa ni Waziri wa Maliasili na Utalii, kwa kuwa waliamua kuwatisha
askari wakati walipodai fedha kiasi cha shilingi laki moja na nusu baada
ya kutangaziwa bungeni kuwa fedha hizo zipo katika resheni yao.
Lema amuonya Membe asiwazie urais
Aliyekuwa Mbunge wa Arusha Mjini, Godbles Lema akizungumza katika
mkutano huo, alisema Waziri wa Mambo ya Nje na Mahusiano ya Kimataifa,
Bernad Membe, amepoteza sifa ya kufikiria kuwa kiongozi wa nchi kutokana
na kushindwa kuusaidia Mkoa wa Lindi kuondokana na umaskini
unaoukabili.
Alisema kama Membe angekuwa kiongozi makini, angetumia fursa yake ya
kusafiri nje kila wakati kutangaza vivutio vya Mkoa wa Lindi na kuufanya
uwe wa kitalii kama mikoa mingine inayosifika kwa utalii Tanzania.
Mnyika awashtukia wabunge wa CCM
Mbunge wa Ubungo, John Mnyika alisema kama Rais Kikwete asipopeleka
bajeti yenye kupunguza mfumuko wa bei katika Bunge lijalo, CHADEMA
itahamasisha nguvu ya umma kumshinikiza afanye hivyo.
Alisema hata kauli inayotolewa na wabunge wa CCM kuwa wataigomea
bajeti ijayo ni ya kujikosha mbele ya jamii, kwa kuwa wanajua wazi suala
hilo haliwezekani kulingana na katiba waliyo nayo.
“Hawa wanasema wataipinga bajeti wakati wana hamu ya kupokea posho za
bungeni, mbona wanajidanganya kwa kuwa wakifanya hivyo rais atavunja
Bunge, na kwa hofu ya matendo yao wengi wanajua hawataweza kurudi, hivyo
hizo ni propaganda tu,” alisema Mnyika.
Sugu aapa kulia na ajira za vijana
Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi, alisema wakati anaelekea
Mtwara akiwa ndani ya ndege, alijua mikoa hiyo ya kusini ni ya kupigiwa
mfano kutokana na aina ya watu aliokuwa nao katika ndege, kwamba hata
vijana wa Mkoa wa Lindi watakuwa wananufaika na rasilimali za mkoa huo.
“Nilipotua nikawauliza kama vijana wananufaika na gesi inayopatikana
katika mikoa yenu, cha ajabu mnaniambia kuwa mnachopata ni vifaa vya
kukingia vichwa na hamruhusiwi kuingia hata katika maeneo ya wawekezaji
kufanya kazi, hili nitakufa nalo bungeni,” alisema Sugu.
Mwenyekiti wa Kijiji avua gamba na kuvaa gwanda
Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Mbanja mkoani Lindi, Issa
Selemani, ameachia nafasi hiyo na kujiunga na CHADEMA, huku akisema
anatafuta haki ya watu wote badala ya kusimamia maslahi ya wachache.
|
No comments:
Post a Comment